USILOPENDA KUTENDEWA USIMTENDEE MWENZAKO




SIMULIZI FUPI - MTENDA HUTENDWA
MTUNZI: GEORGE iron


Umaarufu wake pale chuo cha ualimu Butimba Mwanza, maumbile yake na sauti yake ilikuwa mitego tosha kwa wanaume kujisogeza karibu yake walau wapate kumsabahi kwa sababu yeye hakuwa na utaratibu wa kumsalimia mtu yeyote mpaka umuanze, na ilikuwa nadra sana kukujibu kwa maneno mara nyingi alitumia kichwa au kope zake kujibu salamu hizo, ndio waweza kusema kwamba ungekuwa wewe usingemsalimia lakini kiukweli alikuwa mzuri sana wa kuweza kukuvutia hata wewe, watu walimchukia lakini moyoni walimsifia kwamba alikuwa mrembo wa chati za juu sana.

Umaarufu wa kipekee wa binti huyu ulimfanya awe kama nembo ya chuo kwa wanafunzi, yaani ili uaminike kweli unasomea pale Butimba basi swali la kwanza la uthibitisho lilikuwa, “Unamfahamu Angel??”. Ukiwa

unamfahamu basi kweli unaaminika unasoma chuo kile.
Hakuwa na pesa lakini alivyokuwa anaishi maisha ya juu mh! hutakaa huamini kwamba huko kwao analalia kitanda cha kamba na jamvi ndio godoro lake, huku ikimlazimu kusubiri giza liingie ndio aweze kuoga nyuma ya nyumba yao iliyoezekwa kwa nyasi kasoro chumba cha baba yake ambacho kiliezekwa kwa bati dogo lililochakaa.

Alizaliwa miaka ishirini na moja iliyopita kwa njia za kijadi na kupewa jina la Nyangoko alilokuwa nalo hadi anajitambua na baadaye kujijua na kugundua kuwa lile jina halikuendana na maumbile yake ya kupendeza lakini hakuwa na uwezo wa kulibadilisha lakini licha ya kushindwa kuibadilisha hali hiyo alitumia lazima pale chuoni na ole wako uthubutu kumwita jina hilo (Nyangoko) kama unataka usonywe hadi ujihisi upo uchi basi mwite Nyangoko badala ya Angel (enjo) au malaika kama alivyojibatiza mwenyewe na kulazimisha watu wamjue hivyo kwa hapo chuoni.

Angel alikuwa wakipekee!!!!

Watu walikuwa wanajiuliza kama alilazimishwa kusomea ualimu ama kufeli ndo kulimsukumia njia hiyo, hakika hakuwa akifanania!!!!!

Mguu wa bia uliobebwa na paja lenye unene wa haja, hipsi ambazo zilikuwa zikijibana vyema kwenye nguo zake na kuleta mvuto kumtazama, alijua kutembea vyema hivyo nyama za makalio yake zilitingishika vyema pia. Mwenye macho aliona!!

****

Deogratius au Mtu pori kwa wengi walivyomzoea sio tu kwa jinsi alivyokuwa mshamba hapana pia alikuwa anatoka Morogoro lilipotoka kundi lililovunjika la muziki wa kizazi kipya la watu pori lililopata umaarufu mwishoni mwa mwaka 2006.

Licha ya ushamba wake labda uliochangiwa na umaskini au mazingira aliyokulia Deo bado alikuwa na hisia kali za kimapenzi kama binadamu wengine na kikubwa zaidi alikuwa ameangukia katika kumpenda binti mwenye maringo na mikogo yote pale chuoni (Angel) na aliamua kuchuana vikali na Steward mtoto wa diwani kata ya nyamagana katika kumuwania Angel. Mchuano huo ulikuwa kama kituko kwani dharau aliyoonyesha Angle kwa Deo kwa mwanaume mwingine angekata tamaa au angempiga vibao yule binti.

“Hivi Deo ndugu yangu una marafiki????” siku moja katika maongezi yake na Deo aliulizwa
‘”Ndio ninao tena wengi tu mbona…..kwanini
umeuliza hivyo ???’’ alijibu kwa furaha
“Basi rafiki zako wanafiki ``

``Kwa nini unawaita wanafiki nani huyo mnafiki ???``
"Deo hivi rafiki zako hawajakwambia huna hadhi ya kuwa na mimi? kaulize vizuri wakueleze" lilikuwa ni jibu alilopewa Deo siku alivyomwandikia kaujumbe Angle wakiwa darasani, darasa zima lilimcheka Deo.
Mtu mmoja tu ndio hakucheka nae ni Steward, hakupendezwa hata kidogo na dharau za Angel kwani aliamini Deo alimpenda Angel kweli tofauti na yeye aliyetaka kuonja ladha ya mrembo huyu kitandani kisha aachane naye . alijisikia vibaya pia kwa kuwa Deo alikuwa mwanaume na kijana mwenzake pia hivyo kuaibishwa kwa Deo ilimaanisha aibu kwa wanaume wote.

* * * *
Furaha aliyokuwa nayo siku hiyo hakuna aliyejiuliza kuna nini, Angel kwa mdomo wake alikuwa amemkubalia Deo kimapenzi , alikuwa amekiri makosa yake na kuomba msamaha na alimwomba waonane jioni hiyo guest moja pale jirani na chuo gharama juu yake Angel, kwa Deo hiyo ilikuwa furaha kubwa sana na hakuhitaji hata Angel aombe msamaha kwani alimwona yupo sawa tu na hana hadhi ya kumuomba msamaha.

Saa moja jioni tayari Angel na Deo walikuwa ndani ya chumba kimoja katika nyumba ya kulala wageni (guest), wote walikuwa na furaha huku Deo akiwa na hamu kubwa sana ya kuonja penzi la mwanamama huyu kwa malengo mawili tofauti, kwanza kuitafuta heshima alitambua wazi kwa kufanikiwa tu kulionja penzi la mwanadada huyu ataheshimika kwa tendo hilo la kumpiku mtoto wa diwani kwa kimwana huyu, pili aliamini kuwa Angel alikuwa anamfaa sana kuishi naye kama mke siku moja.

"Kaoge basi mpenzi wangu tupumzike kidogo nina hamu na wewe kweli," akiwa amebana pua Angel alimwambia Deo aliyekuwa pembeni yake, neno mpenzi ni kama lilipiga shoti akili ya kijana huyu kutoka shamba, kama mwizi haraka haraka akazama maliwatoni akimwacha Angel akisugua paja lake lililokuwa wazi kwasababu ya kinguo kifupi alichovaa. Paja lile sio tu lilikuwa laini bali pia ni kama liliongea lugha ya mahaba ambayo mwanaume akiisikia lazima atetereke.


"Atajua mimi ni nani na kamwe hatajutia usiku huu, alijihakikisha kabisa kuwa alikuwa ametakata mwili wake tayari kwa kugusana na mrembo Angel.

Baada ya kumaliza kuoga na kujifuta mwili wake vyema tukio ambalo lilichukua kama dakika kumi na tano, sasa Deo alitoka bafuni tayari kwa mapambano aliyokuwa amepania sana.

"Angel, Angel!"Deo aliita lakini chumbani hapakuwa na mtu wakati anatoka bafuni, Angel hakuwa pale ndani Deo aliangaza kama kuna chumba cha ziada pale ndani lakini hapakuwa na chumba kingine, akili yake ilisimama kwa muda hadi alipokutanisha macho yake na kikaratasi cha kalenda pale kitandani ambacho hakika kilimvutia kukisoma, kwa haraka haraka akakichukua.

“Au ametekwa mtoto wa watu…….dah!!!” alijiuliza Deo kabla ya kusoma yaliyoandikwa pale katika ile karatasi. Cha ajabu na kweli hapakuwa na maandishi yoyote yale zaidi ya tarehe mojawapo kuwa imezungushiwa duara nayo ilikuwa tarehe moja (1) ya mwezi wa NNE. Siku hiyo ya tukio.

Deo alijiuliza nini maana ya ujumbe ule. Mara ghafla akili yake ikapiga kama radi na kuleta majibu. Majibu yaliyomfedhehesha



"Ayaaaa leo siku ya wajinga mh!........ mi mjinga namba moja duniani,..yes!! mimi ni mjinga namba MOJA" aligutuka Deo baada ya kujiuliza na kupata maana halisi ya hiyo tarehe, mfadhaiko ulimkumba na kujikuta akivaa nguo zake kwa aibu kubwa japo alikuwa peke yake pale ndani. Alitazama kushoto na kulia hapakuwa na mtu. Hisia zake zilizokuwa juu sana zikafifiua na kupotea kabisa.

"Nitawaambia nini sasa washkaji ????? " alijiuliza Deo huku akivaa nguo zake.
Hakika alikuwa ameumbuka!!!!

* * *

Kwa furaha tele Angel alichukua tax iliyompeleka hadi ukumbi wa bwalo la magereza ambapo aliahidiwa na Steward kwamba amemwandalia zawadi kubwa sana siku hiyo. Tabasamu halikumuisha usoni kutokana na kituko alichomtendea Deo.

"Yaani ile ndio dawa yake hapo hatanisumbua tena nina uhakika….pumbavu kweli unadanganyika kijingajinga tu…..wapi na wapi mimi kulala na yule mlugaluga, yaani kweli kabisa aende kuninukia kimbuzimbuzi mimi!!!” alikuwa akijiwazia hivyo Angel wakati teksi ikiwa inazidi kuiacha barabara nyuma na kuelekea anapotaka Angel. Wakiwa wamekaribia kufika Angel alimwomba dereva apunguze mwendo ambapo alianza kujipamba uso wake hadi akapendeza kama ilivyo ada akajipulizia na marashi.

Kwa mikogo na manjonjo aliwasili ukumbini na mshehereshaji (MC) aliwanyanyua wageni wapatao 50 kumpokea mgeni rasmi ambao bila kinyongo walisimama na kuanza kumpigia makofi huku vigelegele pia vikisikika kuwatambulisha kina dada waliokuwa pale, kwa kitendo kile Angel alizidisha mikogo huku akitembea kama vile mlimbwende wa kimataifa alijisikia sana mrembo huyu.

Baada ya kufika na kuchukua nafasi yake kama alivyokuwa ameelekezwa na binti aliyewekwa kwa shughuli hiyo Steward alichukua kipaza sauti na kuanza kuzungumza.

"Ndugu wageni waalikwa mabibi na mabwana nachukua fursa hii bila kupoteza muda kumruhusu mpenzi wangu Angel mbele yenu afungue pazia hili na atoe zawadi yake niliyomwandalia kama ishara ya upendo wangu kwake, najua zawadi hii yaweza kuwa ndogo sana kulinganisha na pendo la dhati analonionyesha kwangu lakini naamini ataifurahia,baada ya kuifungua ndipo sherehe itaanza rasmi, napenda kutamka mbele yenu hakuna msichana nampenda kama Angel" aliongea Stewart kisha MC akamwongoza Angel kwa mbwembwe pamoja na fujo za Dj hadi kwenye pazia kubwa ili afungue na kutoa zawadi yake

"Kama sio gari mh!..........au kibajaji maana Sterwad naye….au ndo lile kabati kutoka Denmark alilokuaga ananiambia" alijiwazia Angel huku akizidi kutembea kwa mikogo kuelekea kwenye pazia. Aliamini alikuwa ni msichana mwenye bahati kupita wote duniani. Alitembea kwa pozi zote za kuzaliwa na za kuiga kwani aliamini ni wengi walikuwa wanamwonea wivu, hivyo alifanya kuwakomesha.
“Nawatakoma mwaka huu????!!!!!” alizidi kujishaua.

“Ntahesabu hadi tatu halafu atatufungulia pazia letu mwanadada mrembo Angel….sote tusimame ” Mc alisherehesha, kweli baada ya kuwa amehesabu hadi tatu, Angel akiwa na furaha tele alitelemsha lile pazia "1/4 HAPPY FOOLS DAY" ndio maneno makubwa aliyoyakuta mbele ya ukuta uliokuwa umezibwa na lile pazia





"Aibuuuuuuuu" ukumbi mzima ukazomea wanawake wakaanza kumshushua kwa kutumia maneno, bila kuteleza akajikuta ameanguka chini alitamani azimie lakini hakuzimia, aliombea ardhi ifunguke aingie ndani yake lakini ndio kwanza ardhi ilikakamaa watu wote bila huruma wakaondoka wakamwacha hapo.
Alihaha huku na kule kama mfa maji!!! Aibu ikawa imechukua hatamu. Alikuwa amesahau kabisa aliyomtendea Deo muda uliopita sasa ilikuwa zamu yake!!! Naye ametendwa!!!!

Tena mbele ya umati mkubwa zaidi!!

Amakweli USILOPENDA KUTENDEWA NAWE USIMTENDEE MWENZAKO


Hakikisha una follow hii blog hapo sehemu ya followers ili upate taarifa pindi tu tutakapo weka story mpya na taarifa mbali mbali 
 Pia una weza subscribe katika you tube channel yangu (https://www.youtube.com/channel_/UC3cUYWecDOOHdWEbydLFuYw).

share: https://alvinhabari.blogspot.com 

pia unaweza kuacha e-mail yako hapo sehemu ya e-mail ili uwe unapata taarifa pindi tu nitakapo pandisha mtandaoni. 

No comments

Theme images by konradlew. Powered by Blogger.